MAKHALIFA WA KIISLAM


Makhalifa Amao ni wanne wakuu:






Makhalifa Waongofu:

Baada ya kufariki Mtume (SAW) na kutoacha mtu wa kushika mahali pake ili kuendeleza Uislamu na kuisimamisha dola yake, ilitokea haja kubwa ya kuchaguliwa mtu wa kusimamia mambo ya Waislamu na kuiendesha nchi juu ya misingi aliyoiweka mwenyewe Mtume (SAW), na kwa hivyo Waislamu wakashauriana kuhusu nani atayekuwa khalifa wa Mtume wa Mwenyezi Mungu rehema na amani ziwe juu yake.
Kuchaguliwa Abubakar:
Walikusanyika Maansari chini ya kipaa cha Bani Sa'ida kushauriana kuhusu jambo hili la kumchagua khalifa wa Mtume (SAW), na akasimama katika Maansari mkubwa wa Makhazraj Saad bin Ubada na kuwaeleza Maansari kwa nini wao wanastahiki zaidi kuwa khalifa kutokana na wao, kwa sababu ya kumuamini Mtume (SAW) wakati walipomkataa watu wake, na kumpokea na kumnusuru na kupigana na maadui wa Mwenyezi Mungu mpaka ukasimama Uislamu.
Muhajirina, kwa upande wao, akiwemo Abubakar na Umar na Abu Ubeyda, waliposikia kuwa Maansari wamekutana kujadiliana suala hili la ukhalifa, walikwenda wakajiunga na Maansari na kuinuka Abubakar upande wa Muhajirina na kuwaeleza watu kuwa Muhajirina ni watu wa kwanza waliomuamini Mtume (SAW) na kupata kila aina ya mateso kwa ajili ya Mwenyezi Mungu na Mtumewe, na kukhalifu Waarabu wote ambao wakiamini ushirikina na kuabudu masanamu, na kuwa na Mtume wao katika shida na furaha. Kisha akataja fadhila za Maansari na kuwasifu na kuwaambia kuwa wao ni ndugu zao na hawawezi kukata shauri bila ya wao, lakini Waarabu hawawezi kuwafuata wao kwa sababu wamezowea kuwafuata Makureshi tangu zama za zamani na kwa hivyo viongozi hawana budi kutokana na Makureshi, na Maansari ni mawaziri wao na washauri wao.
Akasimama Al-Hubab bin Al-Mundhir na kuwapigania watu wake Maansari na kuwaambia kuwa nyinyi mna kila kitu, kuanzia mali na silaha na nguvu na ujuzi wa kivita, na kuwa watu wanatazama nini mtafanya wakufuateni, basi msikhitalifiane na kuweni kitu kimoja na hapana yeyote atakayekwenda kinyume na nyinyi, na kwa hivyo, wakitaka atoke kiongozi kwetu na kiongozi kwao.
Umar bin Al-Khattab akaikataa rai hii na kuwaambia kuwa Waarabu hawatakubali wao wawe viongozi ilhali Mtume (SAW) hatokani nao, na kuwa wao Muhajirina ni jamaa zake Mtume (SAW) na vipenzi vyake, na hapana atakayekataa sisi tuwe viongozi baada yake.
Maneno haya hayakumridhisha Al-Hubab na akawashawishi Maansari wasisikilize maneno ya Umar na kuwa wao ni wenye haki zaidi ya Ukhalifa na wakiwa Muhajirina watataka kuuchukuwa kwa nguvu, basi watoeni nchi na piganieni haki yenu, jambo ambalo lilimkasirisha sana Umar na kukakaribia kuzuka mapigano baina ya Al-Hubab na Umar, lakini aliingilia Abu Ubeyda na kuwaambia Maansari: Enyi jamii ya Maansari! Nyinyi mlikuwa watu wa kwanza wa kunusuru Uislamu na kuutia nguvu, basi msiwe watu wa kwanza kubadili na kughairi!
Kauli hii ya Abu Ubeyda iliwatuliza Maansari na kuwafanya wafikirie maneno hayo na hoja hizo. Akasimama Bashir bin Saad katika viongozi wa Khazraj na kusema kuwa ijapokuwa sisi tuna fadhila katika kupigana na Washirikina na kuwa wa kwanza kuinusuru dini hii, lakini sisi hatukutaka haya isipokuwa radhi za Mola wetu na kumtii Mtume wetu, na wala hatutaki starehe za kidunia, kwani neema za Mwenyezi Mungu juu yetu ni nyingi, na tambueni kuwa Muhammad (SAW) ni katika Makureshi, na watu wake ni wenye haki naye zaidi na aula kwake kuliko sisi, na naapa kuwa Mwenyezi Mungu hataniona ninashindana nao katika jambo hili abadan. Basi mcheni Mwenyezi Mungu wala msishindane nao.
Umar baada ya kusikia haya aliitumia fursa hii na kumwambia Abubakar: Nyosha mkono wako ewe Abubakar! Na aliponyosha alimpa mkono na kumchagua kuwa khalifa wa Waislamu na kumwambia: Je, hakukuamrisha Nabii ewe Abubakar kuwasalisha Waislamu, basi wewe ndiye khalifa wa Mwenyezi Mungu na sisi tunakuchagua wewe ili kuonyesha utiifu wetu kwa yule mbora kabisa aliyependwa na Mtume wa Mwenyezi Mungu katika sisi sote.
Akasimama Abu Ubeyda na kumuunga mkono Umar na kumchagua Abubakar huku akisema: Hakika wewe ni mbora wa Muhajirina na wa pili aliyekuwa na Mtume (SAW) katika pango, na mwakilishi wa Mtume (SAW) katika mambo ya dini, basi nani huyo inayempasa kukutangulia au kutawala jambo hili badala yako?!
Kisha wote waliohudhuria hapo wakampa mkono na kumchagua kuwa Khalifa wa Mtume (SAW) na kuonyesha utiifu wao kwake. Huu ulikuwa ni uchaguzi wa watu maalumu kwani waliokuwepo hapo ni Masahaba wakubwa tu peke yao. kisha siku ya pili yake alipokwenda Abubakar msikitini pamoja na Umar, akasema Umar: Hakika Mwenyezi Mungu amelikusanya jambo lenu hili la Ukhalifa kwa yule ambaye ni mbora wenu, sahaba wa Mtume (SAW) wa pili wake aliyekuwa naye kwenye pango, basi simameni na muonyeshe utiifu wenu. Basi wakasimama watu na kumchagua Abubakar.
Baada ya kuchaguliwa Abubakar kuwa Khalifa wa Waislamu, alisimama na kusema: Ama baada ya kumhimidi Mwenyezi Mungu na kumsalia Mtume (SAW). Enyi watu! Mimi nimechaguliwa kukutawaleni wala Mimi si mbora wenu, basi nikifanya vizuri nisaidieni na nikifanya vibaya ninyosheni. Ukweli ni amana na uwongo ni khiyana. Na dhaifu katika nyinyi ni mwenye nguvu kwangu mpaka nimpatie haki yake inshallah, na mwenye nguvu katika nyinyi ni dhaifu kwangu mpaka nichukuwe haki kutoka kwake inshallah. Asiache mmoja katika nyinyi Jihadi katika njia ya Mwenyezi Mungu, kwani watu hawaiwachi hii Jihadi isipokuwa Mwenyezi Mungu huwapa idhlali (unyonge), wala hakuenei machafu katika watu isipokuwa Mwenyezi Mungu huwaletea wote balaa. Nitiini maadamu nitamtii Mwenyezi Mungu na Mtumewe, lakini nikimuasi Mwenyezi Mungu na Mtumewe basi hapana utiifu kwenu juu yangu. Simameni msali Mwenyezi Mungu akurehemuni.
Khalifa wa kwanza: (11H-13H)
Abubakar Assiddiq alikuwa akijulikana kwa jina la Abdul-Kaaba, kabla ya Uislamu, kisha akaitwa na Mtume (SAW) baada ya kusilimu Abdullahi bin Abi Quhafa naye anatokana na kabila la Taym bin Murra bin Kaab naye ni mdogo wa Mtume (SAW) kwa miaka miwili na kitu kwani alizaliwa baada ya kuzaliwa kwa Mtume (SAW) kwa miaka miwili na miezi kidogo.
Utotoni mwake aliishi kama watoto wenzake wa hapo Makka alipozaliwa, lakini alipokuwa kijana aliingilia mambo ya biashara akawa ananunua na kuuza nguo na Mwenyezi Mungu akamfanikia sana katika biashara na kuwa mmoja katika matajiri wa kubwa wa Makka.
Alisifika Abubakar toka ujana wake kuwa ni mtu mwenye heshima kubwa na mtulivu na mpole na karimu na mwenye akili nzuri, na kwa hivyo alikuwa hashiriki katika mambo maovu yaliyokuwa yakifanywa na watu wake hapo Makka kama ya kulewa na mengineyo machafu, na kwa hivyo hajawahi kulewa la katika zama za Ujahili wala za Uislamu, kama alivyoeleza bintiye Aisha.
Abubakar alikuwa akiishi katika mtaa aliokuwa akiishi Khadija, na baada ya kuolewa Khadija na Mtume Muhammad (SAW) na kuishi katika mtaa huo urafiki wao ulikuwa mkubwa na kuzidi kuwa na nguvu, hasa ilivyokuwa wote wawili walikuwa ni watu wenye heshima kubwa na akhlaki njema na kujitenga na mambo mabaya na maovu, na kushiriki katika mambo ya biashara.
Wakeze na wanawe:
Abubakar alikuwa kabla ya kusilimu ana wake wawili Umm Rumaan na Qutayla, na baada ya kusilimu alimuoa Asmaa bint Umeys na Habiba bint Khaarija, na watoto wake wa kiume ni AbdulRahman na Abdullahi na Muhammad na wa kike ni Asmaa na Aisha na Umm Kulthum.
Kusilimu kwake:
Abubakar Assiddiq alikuwa ni katika watu wa kwanza kusilimu baada ya Khadija na Ali bin Abi Talib na Zayd bin Haritha, na akashikamana sana na Mtume (SAW) na kumuamini na kumsadiki mpaka Mtume (SAW) akampa lakabu ya Assiddiq, na akawa katika waliobashiriwa Pepo na Mtume (SAW) na sahibu yake wakati alipohama kwenda Madina.
Baada ya kusilimu alifanya bidii kubwa kuwavutia watu katika Uislamu na katika watu waliosilimu kwa mwaliko wake Uthman bin Affan na Zubeyr bin Al-Awwam na AbdulRahman bin Auf na Saad bin Abi Waqqas na Talha bin Ubeydillah. Aidha, alinunua wengi katika watumwa na kuwawacha huru na kuwasilimisha kama Bilal bin Rabah.
Alisimama Abubakar baada ya kusilimu kwake kumsaidia Mtume (SAW) katika kutangaza kwake dini ya Mwenyezi Mungu tangu mwanzo wa daawa, na aliendelea kumsaidia na kumpa moyo na kumsabilia kwa hali na mali na kuendelea kuwa naye wakati watu walipomkadhibisha wakati wa Israa na Miraji, na kupata nafasi ya kuhama naye wakati alipoamrishwa kuhajiri kwenda Madina na kufanya kila lililomkinika kumsaidia mpaka kuwasili naye Madina kwa salama na amani.
Waziri wa Mtume (SAW):
Alikuwa Abubakar Assiddiq msaidizi mkubwa wa Mtume (SAW) katika vita na amani na siku zote alikuwa naye pamoja na alikuwa ni kama waziri wake, yeye pamoja na Umar katika kumpa mashauri mbali mbali katika mambo ya kidunia, na alionyesha msimamo mzuri katika vita vya Uhud wakati walipokimbia aghlabu ya Waislamu isipokuwa baadhi ya Masahaba akiwemo Abubakar, na kadhalika katika sulhu ya Hudaybia wakati alipokubali Mtume (SAW) masharti ya Washirikina na kukubali kurudi Madina asifanye Umra mwaka ule yakawatia dhiki sana Waislamu haya pamoja na Umar ila Abubakar alisimama naye na kufahamu hekima ya kukubali Mtume (SAW) masharti haya na kuwa ni ushindi kwa Waislamu.
Mwakilishi wa Mtume (SAW):
Katika mwaka wa tisa, Mtume (SAW) alimwakilisha Abubakar kwenda na watu kuhiji huko Makka baada ya kutekwa Makka na kuwa huu ndio mwaka wa mwisho watakaoruhusiwa Makafiri na Washirikina kuhiji hapo Makka, na alipokuwa Mtume (SAW) ni mgonjwa na hawezi kusalisha watu alimwakilisha Abubakar awe imamu wa watu katika Sala zao, na akawa Abubakar ndiye mtu aliyetangulizwa na Mtume (SAW) katika mambo mbali mbali katika uhai wake, jambo ambalo liliwafanya Masahaba kufahamu kuwa hapana anayefaa kushika Ukhalifa isipokuwa yeye baada ya kufariki Mtume Muhammad (SAW).
Fitina ya kwanza:
Baada ya kushika Ukhalifa, alipambana Abubakar Assiddiq na fitina kubwa iliyoenea pande mbali mbali za Arabuni na kuitetemesha dola changa ya kiislamu, kwani baadhi ya watu walidai Utume baada ya kufa Mtume (SAW) na kusababisha mgorogoro na mvurugano mkubwa baina ya Waislamu na makabila ya watu hawa.
Huko Yemen alidai Aswad Al-Ansi kuwa yeye ni Mtume na kudai kuwa anajua elimu ya mambo yaliyofichikana, na kueneza fikra zake kwenye masoko na mahali pa biashara na kufanyia stihzai dini na kuchezea shere mafunzo yake, na kadhalika yakafanywa haya na Maslama huko Yamama, na Talha bin Khuwaylid karibu na Makka.
Vitendo hivi viovu vilisababisha makabila mbali mbali yaliyokuwa na imani dhaifu kutoka katika dini na kukataa kufuata uwongozi wa Madina na wengine kukataa kutoa Zaka, na kujikusanya mabedui na watu wa miji mbali mbali ili kuihujumu Madina na Waislamu, jambo ambalo lilimfanya Abubakar afanye haraka kutayarisha jeshi kupambana na fitina hii na kuukata mzizi wake moja kwa moja.
Waislamu waliingiwa na ghera na kujikusanya kwa haraka sana na kutoka na kiongozi wao Abubakar mpaka Dhul-Qassa, mahali Magharibi ya Madina na kupambana na jeshi la makabila ya karibu na hapo, na baada ya kushinda katika vita hivyo, aliligawanya jeshi lake vikosi kumi na moja na kuvipeleka sehemu mbali mbali za karibu na mbali kupambana na uasi huu na fitina hii.
Kikosi cha kwanza kikiongozwa na Tarifa bin Hajiz kilielekea upande wa Kaskazi-Mashariki ya Madina kwenda kupambana na Banu Suleym na Hawazin. Cha pili kikiongozwa na Khalid bin Al-Walid kilielekea Mashariki kuukomesha uasi wa Talha bin Khuwaylid, kisha kiende kujiunga na kikosi cha kwanza kuwasaidia, na kikosi cha tatu kikiongozwa na Sharahbil bin Hasana kwenda kupigana na Musaylama na kukisaidia kikosi cha Ikrima kilichopelekwa Al-Yamama. Na cha nne kilikuwa kikosi cha Ikrima kilichopelekwa kwa Maslama na kikosi cha tano kilipelekwa kikiwa chini wa uongozi wa Hudheyfa bin Mahsin kwenda Diba Oman kukomesha uasi huko.
Aidha, Abubakar alipeleka kikosi cha sita kikiongozwa na Arjafa bin Harthama kuwaendea watu wa Mahra, na cha saba kikiongozwa na Al-Muhajir bin Umayya kumwendea Al-Aswad Al-Ansi huko Sanaa kumtia adabu na kusitisha uasi na chengine cha nane kilipelekwa Tihama huko Yemen kikiongozwa na Suweyd bin Muqrin, na cha tisa kikiongozwa na Al-Alaa bin Al-Hadhrami kwenda Al-Bahrain na cha kumi ni kikosi cha Amr bin Al-Aas kwenda Kaskazini ya Bara Arabu kuliendelea kabila la Khuzaa, na cha kumi na moja ni kikosi cha Khalid bin Said kuelekea Mashariki ya Sham kupigana na waliortadi huko na kukisaidia kikosi cha Amr bin Al-Aas.
Vikosi hivi vilipata ushindi mkubwa kila sehemu vilipopelekwa isipokuwa kikosi cha Ikrima ambacho kilipelekwa kupigana na Maslama kwa sababu Maslama alikuwa na jeshi kubwa lililokaribia watu 40,000, lakini alipokuja Khalid kumsaidia na kikosi chake wakakimbia wale waliortadi na ukawa ushindi ni wa Khalid. Naye Ikrima alipoona matokeo hayo alimuachia uwongozi Khalid na yeye akaelekea Oman kupambana na Dhu Taj kiongozi wa waliortadi huko na kumshinda kwa msaada wa Hudheyfa na Arjafa. Kisha hawa wakaelekea Shihr na Hadhramaut na Yemen na kukomesha uasi huko. Naye Khalid baada ya kupata ushindi alielekea Al-Bahrain kwenda kumsaidia Alaa Al-Hadhrami ambaye alikuwa amezungukwa na maadui chini ya uwongozi wa Nuuman bin Al-Mundhir, na kuweza kuwashinda maadui wote wa Uislamu.
Mambo muhimu aliyoyafanya:
Baada ya kuwashinda waasi waliortadi na kutoka kwenye dini ya Mwenyezi Mungu na kuwarudisha watu katika njia ya sawa na kuikutanisha dola chini ya utawala wa Uislamu, alifanya kila aliloweza kuipa nguvu dola ya kiislamu na kuuhifadhi Uislamu na Sharia zake na hukumu zake.
Vita vilipomalizika, walikuwa wengi katika Masahaba waliokuwa wamehifadhi Qurani kwa moyo walikuwa wameuliwa katika vita hivi, na ilivyokuwa Qurani wakati wa Mtume (SAW) haikuwa imeandikwa katika kitabu kimoja kama tunavyouona msahafu hivi leo, bali ilikuwa imeandikwa katika ngozi za wanyama na majani ya mitende na juu ya mawe malaini na mifupa na kuhifadhiwa kwenye nyoyo za Masahaba.
Baada ya kuuliwa Masahaba 70 wenye kuhifadhi Qurani yote katika vita vya Yamama, alisimama Umar bin Al-Khattab kumuashiria Abubakar hatari ya kutokusanywa Qurani Tukufu katika kitabu kimoja, lakini Abubakar aliona uzito kufanya jambo ambalo Mtume (SAW) hakulifanya, na akasita kidogo mpaka Mwenyezi Mungu alipoukunjua moyo wake kulikubali jambo hili. Abubakar akamwita Zaid bin Thabit ambaye alikuwa ni mwandishi wa Wahyi wa Mtume (SAW) na mwanachuoni mkubwa wa Qurani na mwenye kuihifadhi yote nzima ili kumtaka aikusanye na kuiandika kwenye kitabu kimoja.
Kukusanywa kwa Qurani:
Zaid bin Thabit naye vile vile kwa upande wake alisita kutekeleza jambo hili mpaka uzito moyoni mwake wa kufanya jambo ambalo Mtume wake hakulifanya kumuondoka, ndipo alipowataka watu wenye maandishi ya Qurani yoyote wayalete kwake pamoja na mashahidi wawili kuthibitisha kuwa maneno haya yaliandikwa mbele ya Mtume (SAW), juu ya kuwa yeye mwenyewe kaihifadhi Qurani nzima, na hii ni kwa sababu ya kuogopea kutia ndani ya Qurani maneno yasiyokuwa ya Mwenyezi Mungu.
Qurani Tukufu baada ya kuandikwa kwenye kitabu kimoja alikiweka Abubakar wakati wa Ukhalifa wake, kisha akakichukuwa Umar katika zama zake na baada ya kufa Umar, msahafu ulibaki katika mikono ya Hafsa bintiye Umar na mkewe Mtume (SAW), mpaka alipotawala Uthman Ukhalifa ndipo alipokichukua na kufanya nuskha na kupeleka miji mengine.
Kulipeleka jeshi la Usama Sham:
Mtume (SAW) kabla ya kufariki alikuwa amemchagua Usama bin Zayd kuongoza jeshi kwenda Sham kupigana na Warumi, lakini hakudiriki kufika mbali, Mwenyezi Mungu akamkhitari Mtume wake na jeshi likarudi kuhudhuria mazishi ya Mtume wao (SAW).
Aliposhika Abubakar Ukhalifa alimuamrisha Usama atoke na jeshi lake na kuelekea Sham kwenda kupambana na Warumi, na ijapokuwa baadhi ya Masahaba walitaka Abubakar amuuzulu Usama kwa udogo wake, kwani alikuwa wakati huo ni kijana wa miaka kumi na saba tu, na kumpa uwongozi sahaba mwengine aliye mkubwa, lakini Abubakar alikataa kumuuzulu mtu ambaye Mtume (SAW) mwenyewe amemchagua, na kwa hivyo likatoka jeshi chini ya uwongozi wa Usama na kupata ushindi mkubwa kabisa dhidi ya Warumi, na kwa hivyo akaweza kuithibitisha mipaka ya dola ya kiislamu iliyopakana na dola ya Warumi.
Vita vya Kaadhima-12H:
Baada ya kwisha kupigana na Waislamu walioasi na kukataa kulipa Zaka, Abubakar alimpeleka Khalid bin Al-Walid kwenda kupigana na Wafursi, na kumuamrisha Al-Muthana bin Haritha kujiunga naye, na kwa fadhila za Mwenyezi Mungu aliweza Khalid kushinda katika vita mbali mbali katika hivyo ni Kaadhima au Dhatus-Salaasil, na baada ya kushinda vita hivi, Abubakar alimuamrisha Khalid aelekee Sham kwenda kusaidia jeshi la kiislamu lililokuwa likipigana huko.
Kutekwa Sham:
Yalipokuwa majeshi ya kiislamu yanapata ushindi huko Iraq na Ufursi, majeshi ya kirumi yalijitayarisha huko Sham kuwahujumu Waislamu, na kwa hivyo akatayarisha Abubakar majeshi manne kupambana na majeshi haya ya Warumi, na kuyaamrisha yaelekee Sham.
Vita vya Yarmuk:
Wakati huu Hiraql, mfalme wa Warumi alikuwa kakusanya jeshi kubwa sana lenye wanajeshi zaidi ya elfu mia mbili kwenda kulipiga jeshi la Waislamu, na akampa Maahan uwongozi wa jeshi hilo.
Jeshi la Waislamu lililojikusanya karibu na mto wa Yarmuk lilikuwa halizidi wanajeshi elfu arubaini, na alikuwa kiongozi wao mkubwa ni Khalid bin Al-Walid, naye akamweka Abu Ubeyda bin Al-Jarrah kuongozi kikosi cha katikati, na kwa upande wake wa kulia akamweka Amr bin Al-Aas na kikosi chake na kwa kushotoni mwake akamweka Yazid bin Abi Sufyan na kikosi chake.
Jeshi hili lilipopambana na jeshi la Warumi lilipata ushindi mkubwa kwa nusura ya Mwenyezi Mungu na wakashindwa Warumi na kuuliwa kiongozi wao Maahan na wengi katika maaskari wake, jambo ambalo liliwatia moyo sana Waislamu na kuwapa nguvu kuendelea na vita vyao dhidi ya Makafiri mpaka wakaiteka Sham.
Nidhamu ya Uwongozi:
Wakati Mtume (SAW) alipokuwa hai, alikuwa yeye ndiye kiongozi wa Waislamu katika mambo ya kidini na kidunia, kwani yeye ndiye aliyekuwa mweka Sharia na hakimu na imamu na amirijeshi na mwenye kuamrisha na mwenye kukataza.
Baada ya kufariki Mtume (SAW), walilazimika Waislamu kutafuta kiongozi mpya atakayemwakilisha Mtume (SAW) katika mambo ya maisha, kwani dini ilikuwa imeshakamilika na aliwachia Mtume (SAW) Qurani na Sunna ili yawe marudio yao wakati wowote watakapohitalifiana.
Ukhalifa:
Nidhamu ya Ukhalifa au uwakilishi wa Mtume (SAW) ilihitajika baada ya kufa Mtume (SAW) na kwa hivyo Waislamu wakarudi kwenye Qurani na Sunna ya Mtume wao kujua nini wafanye ili wamchague Khalifa. Yakawa masharti ambayo lazima yapatikane katika kusimamisha nidhamu hii ni:
1- Shura, yaani kushauriana Waislamu kabla ya kukata uamuzi wowote;
2- Uaminifu, kwa yule mtu ambaye atachaguliwa kuwa ndiye Khalifa wa Mtume (SAW) au kiongozi wa Waislamu, nao hupatikana uaminifu huu kwa kuchaguliwa Khalifa na watu makhsusi kwanza wenye kufahamu Sharia na shuruti za Khalifa, na kisha kukubaliwa Khalifa huyu na watu wote kwa jumla.
Sifa za Khalifa:
Khalifa au kiongozi wa Waislamu anatakikana awe na sifa fulani ili astahiki kushika uwongozi huu, nazo ni elimu, yaani awe na maarifa na dini ya Uislamu na hukumu za Sharia yake, na awe na uadilifu kwa kuwa mnyofu na mwenye akhlaki na tabia njema na mwenendo mwema, na awe na uwezo wa kuendesha na kulinda mambo ya Umma wa kiislamu kwa hekima na busara, na awe ni mkamilifu wa akili na kiwiliwili.
Maliwali:
Tangu wakati wa Mtume (SAW), alikuwa Mtume (SAW) akiwachagua watu kuwa viongozi wa makabila na miji fulani ili wamwakilishe katika kusalisha watu na kukusanya Zaka, na aliposhika Abubakar aliwabakisha Maliwali hawa katika kazi zao walizopewa na Mtume (SAW).
Ukadhi:
Aidha, Mtume (SAW) alikuwa amechagua watu fulani wenye elimu na mambo ya dini na uadilifu kuhukumu baina ya watu wakati wanapohasimiana na kugombana kulingana na hukumu za kisharia zinazotokana na Qurani na Sunna za Mtume wa Mwenyezi Mungu. Aliposhika Abubakar Ukhalifa alimchagua Umar bin Al-Khattab kuwa ndiye kadhi wake wa kuhukumu baina ya watu kwa usawa na uadilifu na kwa kuwa Umar alikuwa ni mtu mnyofu sana na muadilifu na mkali hataki mchezo, alikaa na kazi yake hii miaka miwili bila kujiwa na mashtaka yoyote kutoka kwa watu.
Kufariki kwake:
Abubakar hakuishi sana baada ya kufa Mtume (SAW) kwani ulidumu Ukhalifa wake miaka miwili na miezi mitatu na nusu, kisha Mwenyezi Mungu akamkhitari na kufariki dunia akiwa ni mwenye umri wa miaka 63, na kuzikwa karibu na Mtume (SAW) katika nyumba ya bintiye Aisha.
Abubakar ndiye wa kwanza...
1- Kuweka nidhamu ya Ukhalifa kwa njia ya kushauriana siyo kwa kurithi na kuwaachia umma haki ya kuchagua Khalifa wamtakaye.
2- Kusimamisha vita dhidi ya Waislamu waliortadi na kutoka katika dini na kufanya uasi dhidi ya dola.
3- Kukusanya Qurani Tukufu katika msahafu mmoja baada ya kuwa imeandikwa katika sehemu mbali mbali.
4- Kupeleka majeshi kwenda kuteka nchi za Warumi na Mafursi na kupata ushindi mkubwa.
Khalifa wa pili, 13-23H:
Aliposhikika Abubakar na kuhisi kuwa ajali yake imekaribia, aliona bora kuwaita Masahaba na kushauriana nao kuhusu mtu atakayechukua jukumu la Ukhalifa baada yake, naye aliashiria kuwa atakayefaa kwa kazi hii ni Umar bin Al-Khattab, lakini baadhi ya Masahaba walihisi kuwa Umar ni mkali sana na hana mchezo na kwa hivyo utawala wake utakuwa mgumu na mzito juu ya watu. Pamoja na hayo Abubakar kabla ya kufariki alisisitiza na kushikilia kuwa Umar ndiye atakayefaa kuchukua kazi hii nzito ya kuitia nguvu dola changa ya kiislamu na kushughulikia maslaha ya umma.
Umar bin Al-Khattab:
Alizaliwa Umar Makka kabla ya vita vya Fujar kwa miaka minne, na alikuwa ni mdogo kuliko Mtume (SAW) kwa miaka kumi na tatu, na mamake alikuwa akiitwa Hantama, naye ni kijana anayetokana na Banu Adiy mojawapo ya makabila ya kikureshi.
Wakeze na wanawe:
Umar katika umri wake alioa wanawake tisa nao ni: Zaynab bint Madhuun na Umm Kulthum bint Ali bin Abi Talib na Umm Kulthum bint Jaruul na Jamila bint Aasim na Luhayya na Umm Hakim na Fukayha na Aatika, na wanawe wa kiume ni AbdulRahman na Abdullahi na Zayd mkubwa na Zayd mdogo na Ubeydillah na Aasim na AbdulRahman wa kati na AbdulRahman mdogo na Iyadh. Na wanawake ni Hafsa na Ruqayya na Fatma na Zaynab.
Kusilimu kwake:
Alisilimu Umar kwa kutakabaliwa dua ya Mtume (SAW) ambayo aliomba kwa kusema: Ewe Mola! Upe nguvu Uislamu kwa mmojawapo wa Maumar. (Nao ni Umar bin Al-Khattab na Amr bin Hisham). Basi Mwenyezi Mungu akamtia imani Umar na kumhidi akasilimu baada ya kusikia ndugu yake Fatma na mumewe wanasoma Qurani ambayo walikuwa wakisomeshwa na Khabbab. Baada ya kusoma Aya za mwanzo za Sura ya Taha ilimwingia imani na kutaka kwenda kwa Mtume (SAW) kusilimu.
Kusilimu kwa Umar kulikuwa ni ushindi kwa Uislamu, kwani baada ya kusilimu alidhihirisha Uislamu wake na kutaka Waislamu wajitokeze na kudhihirisha Uislamu wao na kufanya ibada zao kweupe, na ukawa mwanzo wa kudhihiri Uislamu, na Mtume (SAW) akampa jina la Al-Faruq, yaani Mpambanuzi baina ya haki na batili.
Kuhamia Madina:
Umar alikuwa ni mtu shujaa sana na mshupavu na jasiri, na alikuwa ni mkali hamuogopi mtu wala hakubali kuonewa, na kama tulivyomuona wakati wa kusilimu kwake vipi ulikuwa msimamo wake, kadhalika wakati wa kuhamia kwake kwenda Madina, kwani baada ya kuruhusiwa Masahaba kwenda Madina na Mtume (SAW), aghlabu yao walitoka kwa kificho na usiku usiku kuogopa kuudhiwa na Makureshi, lakini Umar alipotaka kwenda Madina aliuvaa upanga wake na kuupachika upinde wake na kushika mishale yake na kuufunga kiunoni mkuki wake na kwenda kwenye Al-Kaaba mbele ya hadhara ya Makureshi na kuizunguka Al-Kaaba mara saba na kusali kwenye Makamu ya Ibrahim, kisha akasimama mbele ya Makureshi na kuwaambia:
Nyuso ziharibike! Mwenyezi Mungu hazidhili isipokuwa hizi pua (ambazo watu huziinua kwa kiburi). Mwenye kutaka kumfanya mamake akose mwana, au mwanawe awe yatima, au mkewe awe kizuka, basi naapambane na mimi nyuma ya hili bonde. Kisha huyo akageuka na kuelekea Madina, akiwa kila mmoja katika waliohudhuria hapo kimya hapana aliyeweza kusema kwi!
Mambo muhimu aliyoyafanya:
Alipofariki Abubakar Assiddiq, majeshi ya kiislamu yalikuwa kwenye mipaka ya Sham na Iraq yakipambana na Warumi na Wafursi. Aliposhika Umar Ukhalifa lilikuwa jeshi la Abu Ubeyd Thaqafi linapambana na Wafursi lakini lilishindwa na kuuliwa amirijeshi wao mahali paitwapo Al-Jisr. Kisha Wafursi wakavuka daraja na kuja mpaka sehemu iitwayo Buweyb karibu na Kufa. Hapo Umar akapeleka jeshi chini ya uwongozi wa Al-Muthana bin Haritha kwenda kuwasaidia wenziwao Waislamu na Mwenyezi Mungu akawapa ushindi mkubwa katika vita hivi vya Buweyb mwaka wa 14H.
Vita vya Al-Qadisiya - 15H:
Baada ya ushindi wa Buweyb, Umar alitaka kuiteka Ufursi na kutaka kwenda mwenyewe na jeshi, lakini Waislamu wakamshauri abakie Madina na badala yake ampeleke mtu mwengine, basi akamchagua Saad bin Abi Waqqas kuliongoza jeshi la Waislamu, na kwa hivyo katika vita vya Al-Qadisiya katika mwaka wa 15H, aliweza Saad kwa kuwafikiwa na Mwenyezi Mungu kuwashinda Wafursi na kumuua amirijeshi wao Rustum.
Kutekwa Madain - 16H:
Saad bin Abi Waqqas hakusita hapo kwani aliwafuata Wafursi na kwenda katika nchi yao na kufika mpaka Madain na kuiteka baada ya kuizingira kwa muda wa miezi miwili. Saad aliingia kumbi za majumba ya Kisra mfalme wa Ufursi na kugeuza kuwa ni mahali pa kusali Waislamu.
Vita vya Nahawand - 21H:
Juu ya kuwa Saad aliiteka Madain, lakini alikuwa hakumpata mfalme wao kwani alikimbia na kwenda kujikusanya na kusimamisha jeshi kubwa kwenda kuchukua kisasi dhidi ya Waislamu. Umar akampeleka An-Nuuman bin Muqrin kwenda kupambana na jeshi la mfalme wa Ufursi, na kwa fadhila ya Mwenyezi Mungu Waislamu waliweza kuwashinda vibaya Wafursi na kupata ushindi uliojulikana kuwa ushindi wa shinda zote, na kwa ushindi huu Waislamu waliweza kuiteka Iraq yote na Ufursi nzima.
Kutekwa Damaskas - 14H:
Baada ya ushindi walioupata Waislamu katika vita vya Yarmuk, majeshi ya kiislamu chini ya uwongozi wa Abu Ubeyda bin Al-Jarrah yalisonga kuelekea Damaskas kwenda kupambana na Warumi huko. Jeshi hili likisaidiwa na majeshi ya Khalid bin Al-Walid na Amr bin Al-Aas na Sharahbil na Qays yaliuzingira mji wa Damaskas siku sabiini mpaka ukasalimu amri na kutekwa bila ya vita, na baada ya kutekwa Damaskas, ikatekwa miji mengine kama Hims na Hamaa na Qinsirin na Laadhiqiya na Halab.
Vita vya Ajnadin - 13H:
Majeshi ya kirumi yalijikusanya Ajnadin mojawapo ya vijiji vya Palestini baina ya Ghaza na Al-Quds na kutaka kupigana na Waislamu, lakini jeshi la kiislamu likiongozwa na Amr bin Al-Aas liliweza kuyashinda majeshi ya Warumi na kuteka miji mengine kama Yafa na Nablus na Aqlaan na Ar-Ramla na A'kka na Sayda na Jubayl na Beirut.
Kutekwa Baitul-Maqdis- 16H:
Jeshi la kiislamu liliendelea kuwashinda Warumi na kuteka miji mengine mbali mbali kama Ghaza na Nablus na Baytu Jibrin na kuendelea mpaka likafika Baitul-Maqdis likiongozwa na Amr bin Al-Aas. Hapo Warumi waligoma kusalimu amri, na jeshi la kiislamu likaendelea kuuzingira mji kwa muda wa miezi minne mpaka Warumi walipoona kwamba hakuna faida ya kuushikilia mji na kwa hivyo wakataka kufanya sulhu na wakaomba Umar mwenyewe aje kupokea funguo za mji wa Jerusalem.
Umar alipokuja kupokea ufunguo wa mji, aliwaahidi kuwa atawapa amani na kuandikiana nao mkataba ambao aliandika ndani yake maneno yafuatayo:
(Haya ndiyo ya amani aliyowapa Umar kiongozi wa Waislamu watu wa Jerusalem. Amewapa amani kwa nafsi zao na makanisa yao na misalaba yao, na kuwa hayatakaliwa makanisa yao wala hayatavunjwa, wala hayatapunguzwa kitu katika majenzi yake wala katika nafasi yake, wala hawatalazimishwa kuacha dini yao wala kudhuriwa yeyote katika wao, na ni juu ya watu wa Jerusalem kutoa jizya kama wanavyotoa watu wa Madain).
Kutekwa Misri - 18-21H:
Baada ya kumalizika kutekwa miji ya Iraq na Sham na Palastini, Umar alimtuma Amr bin Al-Aas aelekee Misri kwenda kupambana na Warumi huko, na baada ya kupita miji mbali mbali akiiteka na kuvishinda vikosi vya kirumi, alifika Ain Shams na kupambana na jeshi kali hapo mpaka akataka msaada kutoka kwa Umar, naye akampelekea jeshi la watu mia nne na lilipofika, alijua kiongozi wa Warumi hapo kuwa hapana hila isipokuwa afanye sulhu na Waislamu na kukubali kutoa jizya.
Kisha akaendelea Amr bin Al-Aas na jeshi lake mpaka wakafika Alexandria ambao ndio uliokuwa mji mkuu wa Misri wa wakati huo, lakini hakimu wa kirumi wa mji huo alikataa kusalimu amri na kwa hivyo Waislamu wakauzingira kwa muda wa miezi minne, kisha wakaamua wauhujumu baada ya kugoma hakimu wake kufanya sulhu, na kwa hivyo wakauteka kwa nguvu mwaka wa 21H. Juu ya hivyo, Amr aliwapa masharti yale yale aliyokuwa akiwapa wale waliokubali sulhu katika miji mengine, na kwa hivyo akawataka watoe jizya, naye akawapa dhamana kuwahifadhia haki zao za ibada na kuyalinda makanisa yao na mali zao.
Maliwali wake:
Uislamu ulipoenea sehemu nyingi katika Ukhalifa wa Umar na zikawa nchi nyingi ziko chini ya utawala wa kiislamu, aliamua Umar kuweka maliwali ili asahilishe mas-ala ya kuhukumu nchi hizi zilizokuwa mbali na Madina, akachagua kutokana na Masahaba wenye kujulikana kwa dini yao na ucha Mungu wao na hekima na busara yao na elimu na ujuzi wao wa mambo ya dini na dunia ili wawe ni wenye kuhukumu baina ya watu kwa uadilifu na wasalishe watu na kuongoza jeshi.
Wawakilishi juu ya mali:
Aidha, aliweka Umar pamoja na Maliwali watu waliowakilishwa kukusanya mali inayotoka katika nchi ikiwa ni Zaka au kodi za mashamba, na walikuwa na kazi ya kuangalia kama Maliwali wanakwenda mwenendo wa sawa kama vile vile Maliwali walikuwa wakiwatazama kama hawa Wawakilishi hawendi kinyume na amri za Khalifa.
Makadhi:
Umar ndiye Khalifa wa kwanza ambaye aliweka Makadhi katika wilaya mbali mbali za kiislamu, na kuwausia wafuate Kitabu cha Mwenyezi Mungu na Sunna za Mtumewe (SAW) katika kutoa hukumu baada ya kuyachunguza mashtaka sawa sawa, na kufanya bidii kusimamisha uadilifu na kufanya usawa baina ya watu.
Idara 20H:
Halikadhalika, Umar ndiye Khalifa wa kwanza kuanzisha mambo ya Idara katika zama zake, kwani aliweka sijili la kuandikia majina ya wanajeshi na mishahara yao, na sijili ya kuandika yote yanayopatikana kutoka wilaya mbali mbali za nchi na kuhifadhiwa katika Baytul-Maal (Hazina ya Dola), na matumizi yake, na aliweka Baytul-Maal katika kila Wilaya ili kukusanya mapato mbali mbali yanayopatikana katika Wilaya hizi.
Aina ya Mapato:
Katika mapato ambayo yalikuwa yakipatikana katika zama za Makhalifa Waongofu ni haya yafuatayo:
1- Kharaji: Nayo ni mali au mapato yanayopatikana kutokana na mashamba yaliyokuweko katika nchi zilizotekwa kwa nguvu na vita, na kubakishwa katika mikono ya wenye nchi hizo.
2- Zaka: Nayo ni mali inayotolewa na Waislamu Matajiri kila mwaka kusaidia Maskini na Mafakiri na wengineo.
3- Jizya: Nayo ni mali inayotolewa na Wadhimi (Wasiokuwa Waislamu wenye kuishi chini ya himaya ya Dola ya kiislamu) na hutolewa na wanaume wenye uwezo katika wao.
4- Ghanima: Nayo ni mali au ngawira inayopatikana na Waislamu kutokana na vita wanavyopigana na wasiokuwa Waislamu.
5- Fayi: Nayo ni mali wanayopata Waislamu bila ya vita.
6- Ushuru: Nayo ni kodi inayokusanywa kutokana na biashara zinazofanywa na Wadhimi na wasiokuwa Waislamu wanaofanya biashara ndani ya dola ya kiislamu, na Wadhimi hutoa nusu ya kumi ya bidhaa na wasiokuwa Waislamu hutoa sehemu kumi ya biashara zao.
Waislamu katika zama za Makhalifa Waongofu walikuwa wakitumia katika biashara zao pesa za kirumi (dinari ya dhahabu) na za kisasani (dirhamu ya fedha), lakini wakitia maneno ya kiislamu kama: La ilaha illa llahu au Muhammadun Rasuulullah.
Nidhamu ya kijeshi:
Katika zama za Mtume (SAW) na Makhalifa wake waongofu ilikuwa nidhamu ya kijeshi ni wanajeshi wapanda farasi, na wanajeshi wa miguu, na kikosi cha mbele, na kikosi kinachotangulia kuchunguza habari za maadui, na warusha mishale, na mpango wao wa jeshi wakati wa vita ni kupeleka kwanza wachunguzi wa habari za maadui, kisha wakati wa mapambano hutangulia kikosi cha mbele na kufuatwa na cha kati na kusimama upande wa kulia kikosi na wa kushoto kikosi.
Kikosi cha wapanda farasi ambacho ndicho kikosi kikubwa kilikuwa kikibeba panga na mikuki na ngao na mipinde na mishale, na kikosi cha miguu ambacho kilikuwa kikikaa nyuma ya wapanda farasi kilikuwa kikibeba panga na ngao na kikosi kinachovitangulia vyote hivi ni kikosi cha wapanda farasi na wanajeshi wake wanavaa vizibao vya chuma na kofia za chuma na kuchukua panga na mikuki, na kikosi cha warusha mishale ilikuwa kazi yake kuwarushia maadui mishale na ni kikosi kinachokusanya wanajeshi mabingwa wa kurusha mishale.
Jeshi la kiislamu lilikuwa likisifikana kwa wepesi wake wa kukimbia na uhafifu wake kuliko majeshi ya kirumi na kifursi.
Kuanzilisha Miji:
Madina ndio iliyokuwa dola ya kwanza ya kiislamu baada ya Mtume (SAW) kuhamia huko na kuijenga jamii ya kiislamu kwa mujibu wa Sharia na Hukumu za Mwenyezi Mungu alizowawekea, na ndio dola iliyoendelea kuwa makao makuu ya Makhalifa Waongofu Abubakar na Umar na Uthman.
Katika zama za Umar, na baada ya kutekwa miji mingi, alianzisha Umar miji mipya kwa kuamrisha maamirijeshi walioiteka miji hiyo kuijenga na kuikuza kutokana na kambi za kijeshi walizokuwa wakiishi pamoja na famili zao.
Mji wa Basra:
Mji huu ulianzishwa na amirijeshi Utba bin Ghazawan mwaka 14H, nao ulikuwa chanzo chake ni kambi ya jeshi yenye vibanda vibanda hapa na pale, lakini baadaye nyumba zikaanza kujengwa na makabila mbali mbali yakaanza kuhamia kutoka sehemu mbali mbali, na haukupita muda ukawa mji mkubwa wenye majumba na masoko na misikiti na majengo mengineo, na kuzidi idadi ya wakaazi wake kutoka wanajeshi mia nane kufikia maelfu ya watu na famili zao. Hii ni kwa sababu ya mahali penyewe ambapo palikuwa ni karibu na Ghuba ya Uajemi na mapitio ya misafara ya biashara.
Mji wa Al-Kufa:
Mji huu ulianzishwa na Saad bin Abi Waqqas kwa amri ya Umar bin Al-Khattab na kumtaka achague mahali patakapokubaliana na tabia ya ujenzi wa kiarabu, na baada ya kuanza kama kambi ya jeshi, ulipanuka na kuimarishwa mpaka ukawa katika miji maarufu na mikubwa ya wakati huo, na kuhamia huko wengi katika Masahaba na Wanachuoni, katika hao ni Ibn Masuud na Ali bin Abi Talib ambaye baadaye aliugeuza mji huu kuwa ndio mji mkuu wa dola ya kiislamu badala ya Madina.
Mji wa Al-Fusttatt:
Mji huu ulianzishwa na Amr bin Al-Aas kwa amri ya Khalifa Umar baada ya kuona Amr kuwa ni mahali pazuri pa kuanzisha mji kwa kuwepo maji na kuwa karibu na jangwa linalounga mji huu na mji mkuu wa Uislamu, na baada ya kupachagua hapa mahali alijenga msikiti na kuweka sehemu mbali mbali kwa makabila ya kiarabu ambayo yalikuja kuhamia hapo, na kuwa kila mtaa unajulikana kwa majina ya wanaokaa mtaa huo na likawa kila kabila lina mkubwa wao ambaye anashughulikia mambo yao na mji ukapanuka na kuwa mkubwa na kujengwa misikiti na masoko na mashamba na kuishi watu kwenye neema kubwa.
Halmashauri:
Kushauriana ni jambo lililohimizwa sana na Uislamu na kuamrishwa ndani ya Qurani, kwani Mwenyezi Mungu (SW) amesema: Jambo lao ni kushauriana baina yao. Q.
Kwa hivyo, tangu wakati wa Mtume (SAW), Waislamu walikuwa daima wakishauriana katika mambo yao, na Mtume (SAW) mwenyewe alikuwa haamui jambo likiwa si amri inayotokana na Mola wake bila kuwashauri Masahaba zake, na kadhalika alifanya hivyo Abubakar zama za Ukhalifa wake, kwani akikabiliana na mas-ala alikuwa akitazama katika Qurani, na akikosa alikuwa akitazama katika Sunna za Mtume (SAW) na kuuliza Masahaba wenzake kama wamemsikia au kumuona Mtume (SAW) ametoa hukumu fulani katika jambo hili au mas-ala haya, na akikosa alikuwa akiwakusanya Masahaba na kuwashauri nini afanye.
Aidha, katika zama za Umar alikuwa akifanya kama hivi, na alikuwa na halmashauri ambayo ilikuwa imekusanya Masahaba wakubwa na Wajuzi wa Qurani waliokuwa wakikutanika na kuzungumzia mas-ala mbali mbali yanayowahusu Waislamu yakiwa hayakutajwa ndani ya Qurani au Sunna ya Mtume wao (SAW), na baada ya kujadiliana kulingana na misingi ya dini ya Uislamu, wakitoa rai yao na Umar alikuwa akikata uamuzi wa mwisho kufuata au kutofuata kulingana na ujuzi na maarifa aliyokuwa nayo ya dini.
Halmashauri hii ilikuwa inajadiliana mambo na mas-ala mbali mbali katika maisha ya Waislamu yakiwa ni ya kijamii au ya kisiasa au ya kijeshi na mengineyo, na katika mambo muhimu sana ya halmashauri hii, ni kule kuchagua Umar watu sita kutokana nayo ili waamue nani atakayeshika Ukhalifa baada yake na akachagua Masahaba ambao Mtume (SAW) amekufa akiwa yuko radhi nao, nao ni Uthman bin Affan na Ali bin Talib na Talha na Zubeyr na AbdulRahman bin Awf na Saad bin Abi Waqqas ili awe mmoja wao Khalifa baada ya kufariki kwake na kumweka mwanawe Abdullahi bin Umar kama mshauri wao tu.
Kufariki kwake:
Baada ya kutawala Ukhalifa muda wa miaka kumi na nusu, na alipokuwa akisali Sala ya Asubuhi, alikuja Abu Luulua Feyruz Mmajusi na kumchoma jambia kwenye kiuno chake na baada ya siku tatu alifariki dunia.
Umar ndiye wa kwanza....
1- Kuweka Halmashauri rasmi ya kushauriana mambo ya dini na dunia.
2- Kutoka usiku na kuchunguza hali za raia wake.
3- Kushika kiboko cha kutia adabu wenye kuasi.
4- Kukusanya Waislamu kusali Sala ya Tarawehe pamoja katika Ramadhani.
5- Kupiga walevi mijeledi thamanini.
6- Kuupanua msikiti wa Mtume (SAW) wa Madina.
7- Kuwatoa Mayahudi Bara Arabu na kuwapeleka Sham na Iraq.
8- Kujenga miji mipya ya kiislamu nje ya Bara Arabu.
9- Kuandika juu ya pesa za kirumi na kifursi maneno ya kiislamu.
Khalifa wa tatu: 23H-35H
Kabla ya kufariki Umar bin Al-Khattab aliwakusanya Masahaba sita ambao anajua kuwa Mtume (SAW) amekufa akiwa yu radhi nao, nao ni Uthman na Ali na AbdulRahman bin Awf na Talha na Az-Zubeyr na Saad bin Abi Waqqas, na kuwataka wamchague mmoja wao ili awe Khalifa baada yake, na kuwaonya wasipendelee jamaa zao wakichaguliwa kuwa viongozi.
Umar aliwapa siku tatu kufikia uamuzi kuhusu jambo hili, na kuwaonya kuwa yeyote atakayeuchukuwa uwongozi kwa nguvu bila kushauriana akatwe kichwa chake, na akamwita Abu Talha Al-Ansari akae tayari na watu khamsini katika jamaa zake kuilinda halmashauri isiingiliwe na mtu yeyote mpaka wapitishe uamuzi wao wa kumchagua mmoja katika wao, na wakishindwa kufikia uamuzi, basi mwanawe Abdullahi bin Umar achague mmoja katika wao, na kama hawakuridhia uamuzi wake, basi wawe pamoja na kundi la AbdulRahman bin Awf.
Kwa hivyo, alipofariki Umar walikutana watu hawa sita na kujadiliana kwa muda mrefu kuhusu nani atakayekuwa Khalifa, na baada ya majadiliano, alikubali AbdulRahman kujitoa asichaguliwe Khalifa lakini asimamie kuchagua atakayefaa kuwa Khalifa, na walivyokuwa wengine walimchagua Ali na wengine Uthman, na baada ya kushauriana na Masahaba wengine alitoka AbdulRahman siku ya nne na kwenda msikitini asubuhi ambako watu chungu nzima walikuwa wamekusanyika, na baada ya kutoa hutuba na kuwauliza watu rai zao, alisimama Saad bin Abi Waqqas na kumhimiza AbdulRahman afanye haraka kuchagua mmoja wao kabla zogo kuzidi ndani ya msikiti.
Hapo AbdulRahman aliuinua mkono wa Ali bin Abi Talib na kumuuliza kama ataendesha mambo kwa mujibu wa Qurani na Sunna za Mtume (SAW), na mwenendo wa Makhalifa wawili waliokuja baada yake, Ali akasema kuwa anatumai kuwa atafanya, basi AbdulRahman akauacha mkono wa Ali na kuushika mkono wa Uthman na kumuuliza kama alivyomuuliza Ali, naye akamwambia kuwa:
Inshallah ndiyo nitafanya. Basi AbdulRahman akauinua mkono wa Uthman juu na kusema: Ewe Mola sikiliza na ushuhudie, kisha akasema: Ewe Mola! Mimi nimejiondoshea jukumu hili kwenye shingo yangu na nimeliweka juu ya shingo ya Uthman. Kisha akamchagua Uthman na wote waliokuwepo msikitini wakamkubali Uthman kuwa ndiye Khalifa wao mpya.
Uthman bin Affan (47KH-35BH):
Uthman bin Affan bin Abil-Aas bin Umayya alizaliwa katika ukoo wa kikureshi na mamake alikuwa ni Arwa bint Kureyz, naye alizaliwa katika mji wa Taif, na alifariki babake alipokuwa anakwenda katika mojawapo ya safari zake za Sham kwenda kuleta biashara na kumwachia mwanawe mali nyingi sana, na akainukia kuwa mfanyibiashara mzuri na akaweza kukusanya mali nyingi na kuwa katika matajiri wakubwa hapo Makka, na kuwasaidia watu wake mpaka wakawa wanampenda sana na kumheshimu.
Alikuwa Uthman ni mtu karimu sana na mara nyingi alimsaidia Mtume (SAW) kwa mali yake katika kuutangaza Uislamu na kusaidia Waislamu kama aliponunua kisima cha Ruma kutoka kwa Myahudi ambaye alikuwa akiwatoza pesa Waislamu kwa maji yake na kuwasabilia wateke bure na vile vile katika kutayarisha jeshi la kwenda kupigana jihadi na mambo mengine mengi ya kusaidia Waislamu, naye alikuwa ni mwenye haya nyingi na heshima kubwa mpaka kusema Mtume (SAW) kuwa Malaika wanamstahi Uthman, na alikuwa akijulikana kwa jina la Dhun-Nurayni kwa kuoa kwake watoto wawili wa Mtume (SAW) Ruqayya na baada ya kufariki akamuoa Umm Kulthum, na ni mmoja katika Masahaba kumi waliobashiriwa Pepo na Mtume (SAW).
Wakeze na wanawe:
Wake wote aliowaoa ni tisa nao ni Ruqayya na Umm Kulthum watoto wa Mtume (SAW), na Naila na Faakhita na Umm Amr na Fatma na Ummul-Banin na Ramla na Ummu Walad. Na alizaa nao watoto wa kiume na wa kike, nao ni Abdullahi mkubwa na Abdullahi mdogo na Amr na Khalid na Abaan na Umar na Al-Walid na Said na Al-Mughira na Abdul-Malik. Na wanawake ni Maryam na Umm Said na Aisha na Umm Abban na Umm Amr na Maryam na Ummul-banin, wakiwa wote ni 17, wanaume ni 10 na wanawake ni 7.
Kusilimu kwake:
Uthman alisilimu mapema baada ya Mtume (SAW) kupata utume akiwa ni kijana mwenye umri wa miaka thalathini baada ya kuzungumziwa ujumbe huu wa Uislamu na Abubakar Assiddiq. Naye alikuwa ni Muislamu mwema na sahaba mkubwa katika Masahaba wa Mtume (SAW) na kuhudhuria aghlabu ya vita vya jihadi alivyopigana Mtume (SAW), na alikuwa ni mfanyibiashara aliyepata ufanisi mkubwa katika biashara zake.
Kuhamia kwake Habasha na Madina:
Uthman alikuwa ni katika Masahaba wa kwanza waliohamia Habasha kwa mara ya kwanza na mara ya pili, yeye pamoja na mkewe Ruqayya binti wa Mtume (SAW), kisha ilipotoka amri ya kuhamia Madina, akafunga safari ya kwenda zake Madina na mkewe, na kwa hivyo amepata fadhila za kuhamia Habasha na Madina pamoja.
Mambo muhimu aliyoyafanya:
Aliendelea Uthman kusonga mbele katika nchi mpya za Makafiri na maadui wa Waislamu na kupigana nao na kuziteka nchi zao ili kuweka amani kwenye mipaka ya dola ya kiislamu iliyofika sehemu mbali mbali za ulimwengu wa wakati huo, kwani alimtuma liwali wake wa Basra Abdullahi bin Aamir kumfuata mfalme wa Ufursi aliyewahi kukimbia katika vita vya Nahawand na ambaye amejizatiti kupigana na Waislamu mpaka akampata na kumuua na kulishinda jeshi lake na kuteka Karman na Sajistaan.
Aidha, katika Ukhalifa wake ilitekwa Tabaristan na Said bin Al-Aas na kuiteka Takharistan amirijeshi mwengine aitwaye Al-Ahnaf bin Qays na akaiteka liwali wa Uthman wa Misri, Abdullahi bin Saad bin Abi Sarh mji wa Ifriqiya (Tunis leo) na Nuba kusini mwa Misri, na akaiteka Habib bin Maslama miji ya Armenia, na kuwa dola ya kiislamu katika zama hizi inatawala sehemu kubwa sana ya ulimwengu wa wakati huu.
Vile vile, aliweza Uthman kwa majeshi yake ya baharini na majemadari wake kuviteka visiwa vya Quprus (Cyprus) na Rodz (Rhodes) na Siqilliya (Cicily) na Kriti (Crete) katika visiwa viliopo kwenye bahari ya Meditarenean, na kuwashinda Warumi katika vita vya Dhatas-Sawari na kuitawala bahari yote ya Mediteranean wao.
Nuskha za Msahafu wa Uthman:
Baada ya kutekwa Armenia, Uthman alimpeleka Hudheyfa bin Al-Yamaan kuwa liwali wake huko na kulikuwa katika jeshi lililoiteka Armenia watu kutoka Sham na Iraq na sehemu nyenginezo na alishangazwa na kustaajabishwa kuona watu wanakhitalifiana katika kisomo chao cha Qurani na kumueleza Uthman habari hii ya hatari, ndipo alipokusanya Uthman maandishi ya Qurani yaliyokuwa kwenye mifupa na ngozi na karatasi na mawe na kuchoma moto zote hizi na kuuchukuwa msahafu ulioandikwa katika zama za Abubakar na ambao ulikuwa kwa Hafsa mkewe Mtume (SAW) na kuamrisha ziandikwe nuskha kutokana na msahafu huu na kutawanywa katika miji mikubwa ya kiislamu.
Kuupanua Msikiti wa Makka-29H:
Alipoona Uthman kuwa Msikiti wa Makka umekuwa hauwatoshi Waislamu ambao idadi yao ilikuwa inazidi kila siku na kutoka kila pande za dola ya kiislamu kubwa, alisimama kuupanua msikiti huu katika mwaka wa 29 wa Hijra.
Fitna ya pili:
Ilizuka fitna kubwa zama za Ukhalifa wa Uthman wakati watu walipoona kuwa Uthman anapendelea watu wa kabila lake la Banu Umayya kwa kuwapa vyeo katika miji mbali mbali ya dola ya kiislamu, na Ali bin Abi Talib alimnasihi sana Uthman kuhusu hatari ya jambo hili, na ikawa watu wamegawanyika mafungu matatu: Wale waliopewa vyeo na kujikusanyia mali chungu nzima na kuishi katika anasa kwenye majumba makubwa makubwa, na wale waliokuwa wakiridhika na kidogo na kuishi maisha yasiyokuwa na anasa na kujiepusha na starehe za kidunia, na wale ambao walikuwa na imani dhaifu na ambao ilikuwa nia yao kutia chokochoko na kuchochea fitna baina ya Waislamu.
Kundi la kwanza lilikuwa ni kundi la Muawiya na jamaa wengine wa Uthman ambao walikuwa wakiishi katika hali ya juu ya maisha, na kundi la pili ni la Ali ambalo lilikuwa likipigania watu wote wawe wanashughulikiwa sawa sawa wasipendelewe hawa juu ya wengine, na kundi la tatu la wachochezi fitna na wenye kutaka kuwagawanya Waislamu lililokuwa likiongozwa na Abdullahi bin Sabaa Myahudi kutoka Sanaa aliyejidai kusilimu na kuichochea fitna hii ambayo mwisho wake ilimpelekea Uthman kuuliwa.
Kuuliwa Uthman:
Ilivyokuwa mali katika Ukhalifa wa Uthman ilikuwa nyingi sana na kukusanyika katika mikono ya Maliwali na viongozi wa miji na matajiri, alisimama Abu Dhar Al-Ghafari na kuwanasihi matajiri wa hapo Madina watoe mali zao kuwapa maskini, na kuendelea kuusia na kunasihi na kwenda huku na huko mpaka akafika Sham na kutangaza mwito wake wa kuwaomba matajiri wawasaidie maskini.
Mwito huu ulipomfikia Muawiya alimwita na kujadiliana kuhusu jambo hili, lakini Abu Dhar alishikilia kuwa mali ni mali ya Waislamu na kila mtu apewe haki yake, basi Muawiya akamwandikia Uthman amwite Abu Dhar Madina na alipokutana naye na kumuuliza mas-ala haya, alijibu Abu Dhar kuwa haiwapasi matajiri kuzuiya mali ya Waislamu mikononi mwao, bali inapasa watoe kuwapa wenziwao maskini. Uthman akamwambia kuwa ni juu yake kutoa katika mali yake tu na kuchukuwa Zaka kutokana na raiya, lakini si juu yake kuwalazimisha kuishi maisha ya kimaskini na kujikhini. Abu Dhar akamwomba Uthman ampe ruhusa aondoke Madina ende akaishi sehemu mbali na Madina, basi akampa ruhusa.
Kwa upande mwengine, alisimama Abdullahi bin Abi Sabaa Myahudi aliyejidai kusilimu kutia chokochoko katika nchi alizozitembelea, nazo ni Misri na Basra na Kufa, na kuwachochea watu wawe dhidi ya Uthman kwa hoja kuwa hafanyi uadilifu baina ya watu na akapata wafuasi wengi, basi wakatoka watu kutoka Basra na Kufa na Misri kwenda Madina kumtaka Uthman ajiuzulu, lakini alipokataa Uthman kujiuzulu na kukubali kufanya matengenezo, walikusanyika wapinzani na kuizingira nyumba ya Uthman na kumzuiya kutoka kwenda kusali na kumnyima maji na chakula.
Wakasimama Masahaba na watoto wao akiwemo Al-Hasan bin Ali na Ibn Abbas na Muhammad bin Talha na Abdullahi bin Zubeyr na Abdullahi bin Salam na Marwan bin Al-Hakam na Abu Hureyra na wengi wengineo wanaokaribia watu mia kumhami Khalifa wao, lakini waasi walikuwa wengi na baada ya kupigana na kuumizwa baadhi ya watoto wa Masahaba, walichoma moto waasi mlango wa nyumba ya Uthman na kuingia ndani kwa njia ya nyumba nyengine iliyokuwa imegusana na nyumba ya Uthman na kumvamia na kumpiga na kumchoma panga na alipojaribu mkewe Naila kumlinda walimpiga panga wakamkata vidole vyake.
Uthman aliushikilia msahafu wake na kuuweka mapajani mwake na huku waasi wamemzunguka huyu anampiga teke, yule anamchocha jambia na mwengine anampiga panga mpaka akaanguka na kukata roho. Masahaba walilia sana kwa kifo chake na kiwiliwili chake kilikaa siku tatu bila kuzikwa, kisha Ali pamoja na Talha na Masahaba wengine wakamchukuwa na kumzika.
Uthman ndiye wa kwanza...
1- Kufanya nuskha za Qurani Tukufu na kuzitawanya katika miji ya kiislamu.
2- Kuupanua msikiti wa Makka (Al-Masjidul-Haraam).
3- Kuweka maaskari wa kulinda mji na kuwapa mishahara wanajeshi.
4- Kuweka nyumba hasa ya kadhi ya kuhukumu baina ya watu.
5- Kujenga merikebu za vita na kuanzisha jeshi la kiislamu la baharini.
6- Kuwapa mishahara waadhini kutokana na Baytul-Mal.
Khalifa wa nne (30H-40H):
Baada ya kuuliwa Uthman bin Affan walikutana Masahaba wakubwa hapo Madina na kushauriana kuhusu nani atakayeshika Ukhalifa baada yake, na wakakubaliana wamchague Ali bin Abi Talib awe ndiye Khalifa wa Waislamu, na baada ya kuchaguliwa na Masahaba wakubwa, Waislamu wengine wakamkubali na kuonyesha utiifu wao kwake.
Ali bin Abi Talib:
Alizaliwa Ali bin Abi Talib Makka kabla ya Utume kwa miaka kumi, na kwa hivyo ni mdogo kuliko Mtume (SAW) kwa miaka thalathini, kwani Mtume (SAW) wakati huo alipopewa Utume alikuwa na umri wa miaka arubaini. Mama yake alikuwa akiitwa Fatma bint Asad bin Hashim, na kwa hivyo Ali alikuwa anatokana na Banu Hashim kutoka kwa baba na mama, na alikuwa ndiye mdogo wa nduguze wa kiume Talib na Aqil na Jaafar. Mtume (SAW) alimchukua Ali kumlea kwa sababu babake alikuwa na watoto wengi na alikuwa si mtu mwenye uwezo mkubwa, na kwa hivyo ulipoteremshwa Wahyi kutoka kwa Mwenyezi Mungu, Ali alikuwa akiishi na Mtume (SAW), na kwa sababu hii akawa ni kijana wa kwanza kusilimu.
Kwa sababu ya kuishi na Mtume (SAW) na kulelewa naye, aliinukia Ali kuwa ni kijana mwenye sifa nzuri na tabia njema na alikuwa akijulikana kwa ufasaha wake na ukarimu wake na ushujaa wake mkubwa, kwani inaelezwa kuwa hakupigana na mtu yeyote miereka ila alimshinda, na hakupambana na mtu yeyote katika vita ila alimshinda na kumuua. Ali alisimama na Mtume katika utangazaji wake wa dini ya kiislamu na alipambana na maadui wa Uislamu katika Makafiri na Washirikina kwa ushujaa mkubwa, na unaonekana msimamo wake huu wa ushujaa katika vita vyote alivyoshiriki, na kule kuthibiti katika vita vya Uhud na Huneyn na kusimama kumhami Mtume (SAW) wakati Masahaba wengine walipokimbia.
Ali alihudhuria vita vyote baina ya Waislamu na Washirikina isipokuwa vita vya Tabuk ambavyo Mtume (SAW) alimtaka abakie Madina kumwakilisha yeye juu ya wakeze mpaka atakaporudi vitani, na alionyesha ushujaa mkubwa kabisa na ujuzi mkubwa wa mambo ya vita wakati alipoiteka ngome ya Mayahudi hapo Khaybar ambayo iliwashinda Masahaba wengine kuifikia. Aidha, ushujaa na hekima yake ilidhihiri wakati alipopambana na nduguze Waislamu ilipozuka fitna ya kuuliwa Uthman katika vita vya "Al-Jamal" na "Siffin", na alikuwa ni mtu mwenye haiba kubwa hasa wakati wa mapambano.
Aidha, Ali alikuwa ni katika Masahaba waliosifika kwa elimu yao kubwa ya dini na ujuzi mkubwa wa fiqhi na hukumu za Sharia za kiislamu, na amesimulia Hadithi 586 kutoka kwa Mtume (SAW) na kutoa fatawa nyingi ambazo Masahaba na Makhalifa walikuwa wakizitumia katika kuhukumu na alikuwa ni msaidizi na mshauri mkubwa wa Masahaba na Makhalifa Waongofu Abubakar na Umar na Uthman. Vile vile alijulikana kwa ukarimu mkubwa hasa kwa watu maskini kwani mara nyingi alikuwa akikitoa chakula chake kuwapa maskini na mafakiri na mayatima. Naye ni katika Makhalifa wanne Waongofu na mmoja katika Masahaba kumi waliobashiriwa Pepo na Mtume (SAW).
Wake zake:
Baada ya kumalizika vita vya Badr, alikuja Ali kwa Mtume (SAW) kumposa bintiye Fatma, naye Mtume (SAW) alifurahi na kumpokea kwa mikono miwili na kumuoza Fatma. Ali aliishi na Fatma peke yake mpaka akafariki na kumzika na alizaa naye watoto wake Al-Hasan na Al-Husein na Muhsin na Zaynab na Umm Kulthum. Aidha, alioa Ali wanawake wengine tisa baada ya kufariki Fatma nao ni Khawla na Layla na Ummul-Banin na Ummu Walad na Asmaa na As-Sahbaa na Umama na Umm Said na Muhayya.
Wanawe:
Mbali na watoto wa Fatma, aliruzukiwa Ali watoto wengine kutokana na wakeze wengine nao ni, katika wanaume ni Muhammad Al-Akbar (Ibnul-Hanifiya) na Ubeydillah na Abubakar na Al-Abbas Al-Akbar na Uthman Al-Akbar na Jaafar Al-Akbar na Abdullah na Muhammad Al-Asghar na Yahya na Aun na Umar Al-Akbar na Muhammad Al-Awsatt. Ama wanawe wa kike ni Ruqayya na Ummul-Hasan na Ramla na Umm Hani na Maymuna na Zaynab As-Sughra na Ramla As-Sughra na Ummu Kulthum As-Sughra na Fatma na Umama na Khadija na Ummul-Kiraam na Ummu Salama na Ummu Jaafar na Jumana na Nafisa.
Hijra ya Mtume (SAW):
Alipokuwa tayari Mtume (SAW) kuhamia Madina baada ya kuamrishwa na Mola wake kuondoka Makka, alimwita binamu yake Ali na kumwambia alale kwenye kitanda chake kuwaonyesha Washirikina kuwa yuko Makka bado, na hii ni kwa sababu Washirikina walikuwa wamepanga njama kutaka kumuua Mtume (SAW) na wakawatumiza vijana wao kutokana na makabila mbali mbali ya kikureshi kushirikiana katika kumuua Mtume (SAW) ili Banu Hashim kabila ya Mtume (SAW) isiweze kuchukuwa kisasi.
Ali akajitolea nafsi yake na roho yake na kujisabilia kwa ajili ya Mtume wake na kulala kwenye kitanda chake na juu ya kuwa Mtume (SAW) alipotoka usiku ule kwenda zake kukutana na Abubakar ili waondoke kuelekea Madina vijana wa kikureshi walikuwa nje ya nyumba wakingojea saa ya kumuingilia Mtume (SAW) na kumuua, lakini Mwenyezi Mungu aliwafunga macho yao na kuwatia usingizi na Mtume (SAW) akapita na kwenda zake na safari yake.
Yaliyotokea zama zake:
Baada ya kuuliwa Uthman bin Affan, alitaka Aisha akiwa na Talha bin Ubeydillah na Az-Zubeyr bin Al-Awwam kutoka kwa Ali kuchukuwa kisasi cha Uthman kwa wale waliomuua kwa dhulma, lakini Ali aliona ni bora kusubiri kidogo mpaka hali ya mambo itulie nchini. Hili halikuwaridhisha Aisha na hawa Masahaba na kwa hivyo wakaamua kuondoka Madina kwenda Makka kwa ajili ya kufanya Umra, lakini kisha wakaelekea Basra, na ikabidi Ali atoke kuwafuata ili kuwakinaisha kwa hoja na dalili kuacha vita na kufanya sulhu, lakini watu wa Abdullahi bin Sabaa waliokuwa katika jeshi la Ali walileta mgorogoro kwa kuanzisha vita na kuwahujumu kina Talha na Az-Zubeyr ili isiwepo sulhu, na vikazuka vita vikubwa mahali paitwapo Al-Khariba karibu na Basra.
Vita vya Ngamia 36H:
Vita hivi vilijulikana kuwa ni vita vya ngamia kwa sababu ya kuwepo Aisha mke wa Mtume (SAW) ndani ya kijumba juu ya ngamia akiongoza vita hivi, na vita vilikuwa vikali na wengi waliuliwa kutoka pande zote mbili akiwemo Talha na Az-Zubeyr na akakatwa miguu ngamia wa Aisha na kuanguka chini, na ushindi ukawa wa Ali bin Abi Talib, na baada ya vita Ali akamchukua Aisha na kumrudisha Madina kwa heshima ambako aliishi kwa amani mpaka ilipofika ajali yake mwaka wa 58H.
Vita vya Siffin 37H:
Sababu ya vita hivi ni kuwa Ali baada ya kushika Ukhalifa aliwauzulu maliwali wote waliowekwa na Uthman bin Affan kwa hoja ya kuwa walikuwa wakijikusanyia mali ya umma na kuishi wao katika starehe, lakini hili halikuwaridhisha maliwali, na Muawiya bin Abi Sufyan akiwa ni liwali wa Damaskas aligoma kuuzuliwa na kudai pamoja jamaa zake kina Banu Umayya kilipizwe kisasi cha kuuliwa Uthman, na kwa hivyo Ali akatoka na jeshi kwenda kupambana naye kwa kutoka kwenye utiifu wa Khalifa na kumuasi kiongozi wa kisharia aliyechaguliwa na umma.
Vita vilikuwa vikali sana na viliendelea muda wa siku mia na kumi na kuuliwa idadi kubwa ya watu pande zote mbili, na likawa jeshi la Ali linakaribia kushinda, ndipo alipojitokeza Amr bin Al-Aas ambaye alikuwa upande wa Muawiya na kuamrisha jeshi la Muawiya liinue misahafu juu ya mikuki yao kutaka vita visimamishwe na ipite hukumu kwa mujibu wa Qurani.
Jeshi la Ali ambalo lilikuwa limekusanya wasomi na wahifadhi Qurani wengi sana waliikubali fikra hii na kumtaka Ali akubali kuhukumiwa na Qurani. Ali alifahamu hila hii na aliwaonya watu wake kwa kujua hila za Muawiya lakini wasisikie, na kwa hivyo akawakubalia.
Hila ya Amr:
Kukubali huku kwa Ali kuhukumiwa baina yake na Muawiya kulileta mchafuko na mgawanyo mkubwa katika kundi la Ali bin Abi Talib na kusababisha kuvunjika nguvu za Ali na kuzidi nguvu za Muawiya, kwani walipoanza kuhukumiwa akiwa kwenye upande wa Ali, Abu Musa Al-Ash'ari na upande wa Muawiya, Amr bin Al-Aas. Na walipokutana baina ya makundi mawili haya na kuzungumza, waliamua kwa hila aliyoitumia Amr bin Al-Aas wawauzulu wote wawili Ali na Muawiya na achaguliwe na Waislamu Khalifa wanayemtaka, na wakakubaliana kuwa aanze Abu Musa kumuuzulu Ali, na baada ya kufanya hivyo, alisimama Amr na kumthibitisha Muawiya na kumchagua yeye kuwa ndiye Khalifa na alifanya hivyo kutokana na ahadi aliyopewa na Muawiya kuwa atampa uliwali wa Misri ambao aliuzuliwa na Uthman wakati alipokuwa Khalifa.
Wakati jambo hili linafanyika Ali alikuwa yuko Kufa huko Iraq anangojea hukumu ipitishwe, na kundi lake lililokuwa naye liliposikia kuwa ameuzuliwa lilimkasirikia na kumlaumu kukubali kuhukumiwa hasa ilivyokuwa yeye ni Khalifa wa kisheria aliyechaguliwa na Waislamu na kwa hivyo fitna mpya ikazuka na watu katika kundi lake wakatokana naye na kuunda kundi lililokuja kujulikana kama "Al-Khawarij" yaani wale waliotokana na Ali, na kusababisha kundi hili balaa kubwa, kwani liliwakataa wote Ali na Muawiya na kuanza kufanya fujo na ghasia na kupigana na akasimama Ali kuwarudisha katika njia ya haki wasisikie ikabidi kupigana nao katika mahali paitwapo "An-Naharawan" mpaka akawashinda na kuvunja nguvu yao.
Kuuliwa kwake 40H:
Ali alibaki Al-Kufa huko Iraq na kuufanya mji wa Al-Kufa kuwa ndio mji mkuu wa dola ya kiislamu badala ya Madina, na kuwahimiza watu wa Sham kupigana na Muawiya, lakini Muawiya alikuwa ni mtu mwenye siasa kubwa na aliweza kuwatia mkononi watu wa Sham, lakini Makhawarij hawakunyamaza kwani walipanga njama na kutuma watu watatu kwenda kuwaua Ali na Muawiya na Amr, akapelekwa AbdulRahman bin Muljim kwenda Al-Kufa kumuua Ali, na mwengine kwenda Sham kumuua Muawiya, na wa tatu kwenda Misri kumuua Amr.
Katika hawa watatu aliyefanikiwa kuua ni mmoja tu, kwani yule aliyekwenda kwa Muawiya aliwahi kumjeruhi tu akakamatwa, na yule aliyekwenda kwa Amr alimuua mtu mwengine badala ya Amr akidhani kuwa ndiye Amr, lakini aliyetoka kumuua Ali alimwahi akiwa anatoka kwenda kusali Alfajiri siku ya Ijumaa tarehe 17 ya Ramadhani mwaka wa 40 wa Hijra akamtia jambia la sumu na akafariki baada kupita siku tatu akiwa amekufa shahidi.
Ali alizikwa Al-Kufa akiwa ametimiza miaka sitini na tatu na kukaa katika Ukhalifa kwa muda wa miaka mitano, na kwa kufa yeye zikamalizika zama za Makhalifa Waongofu ambao walikuwa wakifuata Qurani na mwenendo wa Mtume (SAW) katika maisha yao na utawala wao.
Ali ndiye wa kwanza...
1- Kuhamisha mji mkuu wa dola ya kiislamu kutoka Madina kuupeleka Al-Kufa huko Iraq.





Hakuna maoni

Inaendeshwa na Blogger.